banner

Friday, May 9, 2014

Mzimu wa katiba wahamia bunge la bajeti

Mzimu wa Bunge la Katiba umeanza kulizunguka bunge la bajeti, baada ya Mwenyekiti wa kambi ya upinzani bungeni jana, Freeman Mbowe, kuwasilisha hotuba yake yenye madai mengi kuhusu bunge la katiba.

Mbowe alitoa madai hayo wakati akisoma taarifa ya kambi ya upizani katika mkutano wa bajeti ya mwaka wa fedha 2014/2015 unaoendelea mjini Dodoma.

Mbowe alidai mchakato wa bunge maalum la katiba umetawaliwa na CCM na kusema kamwe wajumbe wa bunge hilo kutoka Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) hawatarudi bungeni kujadili katiba, akisema hawakubali kuwa sehemu ya wasaliti wa Watanzania.

Alisema umoja huo utarejea kujadili katiba kama tu rasimu ya katiba itaheshimiwa huku wajumbe wakiheshimiana.

Aidha alidai kati ya wajumbe 201 walioteuliwa kuunda bunge la katiba, 160 ni wanachama na makada wa CCM.

Kuhusu bajeti ya bunge maalum, alisema haikuidhinishwa na bunge na wala wabunge hawana taarifa.


Alisema bunge halifahamu chochote kuhusu gharama zilizotumika na bunge maalum la katiba na halifahamu gharama itakayotumika katika mkutano ujao wa bunge hilo.

Mbowe aliitaka serikali kuanisha bajeti nzima ya bunge maaalum, fedha ambazo tayari zimeshatumika,  nani alijadili na kupitisha bajeti hiyo na lini na kwa haraka gani Mkaguzi wa Fedha (CAG) aliidhinisha na kupitisha matumizi hayo.

Aidha, alivishutumu vyombo vya habari vya umma (TBC1 na TBC Taifa) na magazeti ya Daily News na Habari Leo kwa kuipendelea CCM na makada wa chama hicho, wakati vinaendeshwa kwa kodi ya wananchi, huku akisema hana tatizo na gazeti la Uhuru kwa sababu linamilikiwa na CCM na vyombo vya habari vya binafsi.

Awali Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema Watanzania wana kila sababu ya kuutetea Muungano wa Tanzania, kwani ndio wenye hadhi ya utanzania wao.

Alisema  Watanzania wana kila sababu ya kuikubali miaka 50 ya Muungano kwa vile asilimia 90 ya Watanzania wamezaliwa katika mfumo wa muungano wa serikali mbili na wana kila sababu ya kuulinda na kuutetea.

Alisema kutokana na hali hiyo ndio maana serikali imeamua kuandaa mchakato wa katiba ambao utaangalia namna ya Watanzania watakavyofaidika na hazina ya nchi yao.

Alisema serikali ina imani kubwa mchakato huo utaenda vizuri baada ya awamu ya kwanza kumalizika na kuihakikisha Tanzania katiba iliyo bora.

Aidha alisema serikali inaendelea na mchakato wa vitambulisho vya taifa ambao tayari,umeibua changamoto mbali mbali ambazo serikali inakabiliana nazo.

Alisema shughuli za kiuchumi zimeongezeka na kufanya pato la taifa kuongezeka huku kukiwa na  mahitaji makubwa ya kijamii kwa kuwa hali ya utegemezi nchini bado ni kubwa kutokana na kuwapo kwa kiwango kikubwa cha vijana na watoto yatima.


Alisema pamoja na mfumko wa bei kupungua kutokana na bei za vyakula kuwa katika hali ya wastanI, bado hali ya umasikini hairidhishi kwa Watanzania walio wengi.

Socializer Widget By Blogger Yard
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →

0 comments:

Post a Comment