banner

Tuesday, May 6, 2014

Chama cha akina Zitto Kabwe ( ACT-Tanzania ) chapata usajili wa kudumu.....Yadaiwa Dr. Kitila Mkumbo ni mwanachama mwanzilishi na Zitto Kabwe ni mlezi


CHAMA  cha  siasa  cha  Alliance  for  Change  and  Transparency ( ACT-Tanzania )  ambacho  kinatajwa  kuasisiwa  na  mwanasiasa  machachari, Zitto Kabwe  na  vigogo  wa  zamani  wa  CHADEMA, jana  kilipatiwa  usajili  wa  kudumu  na  msajili  wa  vyama  vya  siasa  nchini,Jaji Francis  Mutungi....

Jaji  Mutungi  alikabidhi  cheti  cha  usajili  wa  kudumu  kwa  kaimu  mwenyekiti  wa  chama  hicho, Kadawi Limbu  katika  hafla  iliyofanyika  mjini  Dodoma  jana....

Kuhusishwa  kwa  Zitto  Kabwe  na  ACT-Tanzania
Habari  za  kuaminika  kutoka  ndani  ya  chama  hicho  zinaeleza  kuwa  Zitto  ambaye  ni  mbunge  wa  Kigoma  kaskazini  kupitia  CHADEMA  ndiye  mlezi  wa  chama  hicho....

Pia  mjumbe  wa  zamani  wa  kamati  kuu  ya  CHADEMA,Dr. Kitila  Mkumbo  naye  anaelezwa  kuwa  mwanachama  mwanzilishi  wa  chama  hicho....

Zitto  na  Kitila  wanahusishwa  na  chama  hicho  baada  ya  kuvuliwa  uanachama  wa  CHADEMA  Novemba  22  mwaka  jana  kwa  kutuhumiwa  za  kula  njama  za  kuhujumu  chama  hicho....

Hata  hivyo  Zitto  alipinga  uamuzi  huo  na  kuamua  kufungua  kesi  mahakama  kuu  kupinga  kuvuliwa  uanachama  wake...

Ukweli  wa  Zitto  kuwa  karibu  na  chama  hicho  unajionyesha  zaidi  kutokana  na  wadhifa  wa  katibu  wa  muda  wa  ACT-Tanzania  kushikwa  na  Samson  Mwigamba,ambaye  alivuliwa  vyeo  vyake  kutoka  CHADEMA  pamoja  na  Zitto  na  Dr. Mkumbo  kwa  tuhuma  zinazofanana....

Bila  kusahau  kuwa  wanachama  wengi  wa  ACT-Tanzania  wanaelezwa  kuwa  wanatoka  katika  baadhi  ya  mikoa  ambayo  ilikuwa  chini  ya  Zitto,wakati  alipokuwa  mwenyekiti  wa  CHADEMA  kanda  ya  magharibi...

Alipoulizwa  juu  ya  habari  ya  Zitto  kuwa  mlezi  na Kitila  kuwa  mwanachama, Mwigamba  hakukiri  wala  kukataa  juu  ya  jambo  hilo....

"Hayo  mambo  ya  nani  ni  mwanachama  wetu  kwa  sasa  siwezi  kuyazungumzia.Jambo  muhimu  hapa  tumepata  usajili  wa  kudumu" Alisema  Mwigamba  ambaye  alijibu  kwa  nia  ya  simu  kutoka  Arusha  ambako  alikuwa  kwa  shughuli  binafsi  na  kumfanya  akose  shughuli  ya  kukabidhiwa  cheti  cha  usajili...

Msajili  ataka  siasa  za  ukomavu
Akizungumza  kabla  ya  kukabidhi  cheti  hicho, Jaji  Mutungi  aliwataka  viongozi  wa  chama  hicho  kufanya  siasa  zenye ukomavu  kwa  kuzingatia  sheria  ya  vyama  vya  siasa  na  kanuni zake

Jaji  Mutungi  aliwataka  pia  viongozi  hao  kuwaheshimu  wanachama  wao  kwa  kuwa  vyama  vingi  vikishapata  usajili  viongozi  huwasahau  wanachama  wao....

"Mmepata usajili, mmeikuta  nchi  yetu ina  amani  hivyo  tunaomba  mfanye  siasa  ambazo  zitahakikisha  nchi  inaendelea  kuwa  na  amani,"  alisema Jaji  Mutungi  akitaka  chama  hicho  pia  kishiriki  katika  kutoa  maoni  ya  kuzifanyia  marekebisho  sheria  ya  vyama  vya  siasa  na  sheria  ya  gharama  za  uchaguzi

Kwa  upande  wake  msaidizi  wa  msajili  wa  vyama  vya  siasa,Sisty Nyahoza,aliipongeza  ACT-Tanzania  kwa  kutimiza  masharti  na  hatimaye  kupata  usajili  wa  kudumu...

Alisema  chama  hicho  kilifanikiwa  kuleta  wanachama  zaidi ya  200  katika  mikoa  10  ya  Tanzania   Bara  na  mikoa  miwili  kutoka  Tanzania  Visiwani...

"Epukeni  kujihusisha  katika  vurugu, sheria inakataza  vyama  vya  siasa  kutumia  nguvu  katika  shughuli  za  siasa,hali  hiyo  inafifisha  demokrasia  na  kuwatia  hofu  wanachama" alisema

Akizungumza  mara  baada  ya  kupokea  cheti  cha  usajili  wa  kudumu,Limbu  alisema  chama  hicho  kimepanga  kufanya  demokrasia  ya  kweli  nchini...

"Chama  chetu  hakitakuwa  chama  cha  vurugu,kitakuwa  ni  chama  cha  heshima,hakitakuwa  na  mmiliki,kitakuwa  ni  chama  cha  wanachama, hatutegemei  migogoro  na  tutafanya  siasa  za  kistaarabu" Alisema  Limbu

Akizungumzia  chama  hicho  kuwa  na  watu  maarufu  nyuma yake,Limbu  alisema  hayo  ni  masuala  ya  kusikia.

"Sisi  ni  wanasiasa  wazoefu,tunajiamini,hatuna sababu  ya  kufanya  kazi kwa  kuwa  kuna  watu  nyuma  yetu  wanategemewa  kuwa  viongozi"

"Tunaamini wapo  watu  na  viongozi  wa  vyama  vingine  wanakerwa  na  demokrasia  ndani  ya  vyama  vyao,vipo  vyama  ambavyo  ni  makampuni  ya  watu, ukionekana  kugusa  maslahi  ya  mtu  unafukuzwa, tunawakaribisha  waje  tujenge  demokraia.

"Tunaamini  watu  wa  namna  hiyo  ni  moja  kati  ya  chachu  ya  watakaokuja  kujenga  chama  chetu,tunamhitaji  mtu  yeyote  mwenye  uwezo  na  nguvu, atakayejenga  demokrasia  ya  kweli" alisema

ACT  yaanza  na  wanachama  4,200
Mwigamba  alisema chama  hicho  chenye  mlengo  wa  kati-kushoto  kina  wanachama  4,200  kutoka  mikoa  13  ya  Tanzania  Bara  na  Zanzibar....

"Chama  chetu  kinaamini  katika  ujamaa  na  demokrasia  jamii,yaani  tunataka  kurudisha  u-Nyerere"  alisema  Mwigamba  ambaye  alitaja  kauli  mbiu  ya  chama  hicho  ni 'Tanzania  Kwanza,Uwazi  na Mabadilko'

Socializer Widget By Blogger Yard
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →

0 comments:

Post a Comment