banner

Tuesday, May 6, 2014

Kiongozi wa Boko Haram asema atawauza wanafunzi wa kike aliowateka nyara....“Nimewateka nyara wasichana wenu. Nitawauza sokoni, kwa jina la Mungu.”


Hofu inazidi kutanda nchini Nigeria na matumaini ya kuwapata wanafunzi wa kike zaidi ya 200 waliotekwa nyara na kundi la Boko Haram yanapungua baada ya kiongozi wa kundi hilo kutangaza kuwa amepanga kuwauza.

“Nimewateka nyara wasichana wenu. Nitawauza sokoni, kwa jina la Mungu.” Alisema kiongozi wa Boko Haram, Abubakar Shekau kwenye video ambapo aliongea kwa lugha ya Hausa na tafsiri yake imetolewa na CNN.

“Kuna soko la kuuza binadamu. Mungu anasema inabidi niwauze. Ameniamuru niwauze. Nitawauza wanawake. Huwa nauza wanawake.” Aliongeza mtu huyo.

Takribani watu 1,500 wameuawa mwaka huu na kundi hilo ambalo maafisa wa Marekani wameeleza kuwa linasaidiwa kimafunzo na watu wenye uhusiano na kundi la Al Qaeda.

Kundi hilo limedai linawateka wanafunzi wa kike ikiwa ni mkakati wao haramu wa kupinga elimu ya magharibi.

Wananchi nchini Nigeria wameendelea kuandamana wakiishinikiza serikali kuharakisha mpango wa kuwaokoa na kuwalinda watoto wao na kundi hilo hatari.

Rais wa Nigeria, Goodluck Jonathan amesema atafanya awezalo kuwaokoa wasichana hao.

Socializer Widget By Blogger Yard
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →

0 comments:

Post a Comment