banner

Tuesday, April 29, 2014

Polisi wakamata silaha tatu za kivita

  Jeshi la polisi mkoani Arusha limefanikiwa kukamata bunduki tatu za kivita zilizokuwa zikitumiwa na wananchi wa kabila la Wasonjo na Wamasai kinyume cha sheria, wilayani Ngorongoro katika mapigano mbalimbali yaliyosababisha vifo na majeruhi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda wa polisi mkoani hapa, Liberatus Sabas, alitaja silaha hizo kuwa ni  SAR yenye namba 20034823 ikiwa na risasi saba, SMG yenye namba NH-4200 ikiwa na magazine yenye risasi tano na G3 yenye namba D60365 ikiwa na magazine yenye risasi tano.

Kamanda Sabas alisema kukamatwa kwa silaha hizo kumetokana operesheni kambambe ya jeshi hilo kwa kushirikiana na wazee wa ukoo wa makabila mawili ya Wasonjo na Wamasai katika vijiji vya Olorien na Mgongo, wilayani humo.

Alisema operesheni hiyo imekuja kufuatia mapigano ya mara kwa mara ya kulipiza kisasi baina ya makabila hayo, ambapo watu wa kabila la Wasonjo mnamo Aprili 8 mwaka huu  walivamia gari aina ya Landrover linalodaiwa kumilikiwa na Wamasai na kulishambulia kwa risasi.


Aliongeza kuwa tukio hilo lilisababisha vifo vya watu wawili akiwemo mwanafunzi wa kidato cha tatu na kuwajeruhi wengine saba wakitoka kwenye vijiji vinavyokaliwa na Wasonjo.

Alisema tukio hilo lililenga kulipiza kisasi kwani kabla ya tukio hilo mtu mmoja wa kabila la kimasai aliuawa wakati akitokea katika kijiji cha Olorieni.

Alisema baada ya mapigano hayo ambayo yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara wilayani humo,   jeshi la polisi  kwa kushirikiana na timu ya wazee wa kimila kutoka makabila yote mawili waliunda tume ya usuluhishi na kufanikiwa kupatikana silaha hizo.

Alisema timu hiyo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kurejesha hali ya amani katika vijiji hivyo kwani baadhi ya wananchi walikubali kusalimisha silaha zao walizokuwa wakitumia katika mapigano mbalimbali  ya makabila hayo mawili.


Alisema timu hiyo itasaidia kupatikana amani ya kudumu baina ya makabila hayo hasimu kutokana na kujikita kwenye utatuzi wa migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikileta msunguano wa mara kwa mara na kusababisha mapigano ya silaha za moto na jadi.

Socializer Widget By Blogger Yard
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →

0 comments:

Post a Comment