banner

Saturday, April 26, 2014

Mwanamke achomwa kisu kisa mume wa mtu.....Aliyemchoma ni mwenye mume, kisu chazama na kukatikia ndani


JESHI la polisi mkoani Tabora  linamshikilia mwanamke aliyejulikana kwa jina la Pima Mabubu kwa tuhuma za kumchoma kisu mpaka kumjeruhi vibaya mwanamke mwenzake, Amina Hussein akidai ana uhusiano wa kimapenzi na mumewe, Adam Ndekeja...

Tukio hilo lililowaacha watu vinywa wazi, lilijiri Aprili 22, mwaka huu shambani katika Kijiji cha Kigwa, Kata ya Ukondamoyo wilayani Uyui, Mkoa wa Tabora.
 
KISU KILIVYOFANYA KAZI

Habari kutoka kwa baadhi ya mashuhuda zinasema kuwa, Amina alichomwa kisu mara mbili, kwenye paja mguu wa kushoto kisha kwenye mgongo ambapo kilizama na kutoka mpini tu!








Amina Hussein akikimbizwa hospital baada ya kupatwa na mkasa huo.

KISA KINASIMULIWA
Kwa mujibu wa taarifa za awali, siku ya tukio, Pima alitoka nyumbani kwake na kumfuatilia mumewe huyo kwenye shamba la tumbaku la kaka wa Amina (jina halikupatikana) ambako alisikia kuwa mwanamke huyo yupo na mumewe.

“Pima alisikia Amina ana uhusiano na mumewe. Siku hiyo akasikia wapo shambani. Akatoka nyumbani na kufuatilia akijua atawanasa laivu,” kilisema chanzo hicho.




Kisu kinachosadikika kilitumika kumjeruhi Amina Hussein.


MWANAMKE ALIYECHOMWA KISU
Akizungumza akiwa amelazwa akiuguza majeraha katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora, Kitete, Amina alisema:

“Mimi sina uhusiano na huyo mwanaume jamani. Kwanza huyo mwanamke simjui kabisa. Nimemwona kwa mara ya kwanza siku hiyo ya tukio.

“Siku hiyo mimi na mwanangu kichanga (wa miezi mitatu) tulikuwa shambani, mimi nilikuwa nikimsaidia kaka yangu kuvuna tumbaku, akaja Adam (mwenye mke) naye akawa anasaidia kuvuna. Kuna wakati nilikwenda kupumzika mahali ili nimnyonyeshe mwanangu.








“Ghafla aliibuka huyo mwanamke. Nilimwona akinifuata mimi moja kwa moja. Aliponifikia alinirukia na kuanza kunichoma kisu mgongoni na kwenye paja la kushoto.

“Ilikuwa ni hatua chache tu tokea mahali ambako mume wake alikuwa akivuna. Nilipiga kelele za kuomba msaada, mume wake akaja mbio kusaidia kwa kumdhibiti mke wake asiendelee kunichoma kisu zaidi,” alisema Amina.

Akaendelea: “Nilianguka chini na kuanza kugalagala huku damu nyingi zikinitoka. Ndipo wasamaria wema nao walifika na kumkamata Pima, wakamfunga kamba na kumpeleka ofisi ya kata ambako alipelekwa Kituo Kikuu cha Polisi Tabora.”

BODABODA YAMKIMBIZA HOSPITALI
Habari zaidi zinasema kuwa, Amina akiwa hoi na damu chapachapa, alipandishwa kwenye bodaboda na kukimbizwa kweynye hospitali ya rufaa ya mkoa kwa ajili ya matibabu huku hali yake ikionekana si ya kuridhisha.

KILA MTU NA WAKE
Taarifa zaidi zinasema kuwa, wakati ndugu wa Amina wakihaha kumshughulikia majeruhi huyo kupata matibabu kwa lengo la kuokoa uhai wake, baadhi ya ndugu wa Pima walipiga kambi nje ya kituo cha polisi wakipigania kumdhamini ndugu yao huyo.

“Ukitaka kujua msemo kwamba kila mchuma janga hula na wa kwao fuatilia mkasa huu. Wakati ndugu wa Amina wakihaha kuokoa maisha yake hospitalini, ndugu wa Pima nao walikuwa wakihangaika kuhakikisha mtuhumiwa huyo anapata dhamana ili arejee uraiani. Hakuna aliyekwenda kumjulia hali Amina,” kilisema chanzo.

KUHUSU MUME WA MTUHUMIWA
Katika hali isiyotarajiwa, mume wa mtuhumiwa huyo alikimbia kusikojulikana muda mfupi baada ya mkasa huo kutokea jambo ambalo limezua maswali yasiyo na majibu.

Wengi wamekuwa wakiuliza ni nini kimemkimbiza mwanaume huyo kama kweli yeye hana uhusiano wowote na mwanamke huyo?!

“Au kuna ukweli unafichwa? Kama hakuna ni kwa nini Adam alikimbia? Hapa kuna haja ya jeshi la polisi kumsaka mwanaume huyo mpaka kumkamata ili ukweli ujulikane,” alisema mkazi mmoja wa eneo hilo.

Credit: Risasi Jumamosi/ GPL

Socializer Widget By Blogger Yard
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →

0 comments:

Post a Comment